Loading...

Mkutano wa wakilishi Z'bar kuanza Jumatano bila CUF


 Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar (BLW ) wataanza kukutana katika mkutano wa kwanza Machi 30, mwaka huu, bila ya Kambi ya Upinzani kuwapo baada ya Chama cha Wananchi (CUF) kususia uchaguzi mkuu wa marudio visiwani humo.
 
Akizungumza na waandishi wa habari Chukwani mjini hapa jana, Katibu wa Baraza, Dk. Yahaya Khamis Hamad, alisema matayarisho ya kikao hicho yamekamilika.
 
Alisema Rais wa Zanzibar, Dk. Ali Mohammed Shein, ameitisha kikao hicho cha kwanza tangu kufanyika kwa uchaguzi mkuu wa marudio na kupatikana wajumbe wa baraza hilo.
 
Alisema kazi kubwa kwa wajumbe itakuwa kumchagua Spika wa Baraza la Wawakilishi, lakini alisema mpaka jana chama kimoja tu ndicho kilichokuwa kimerejesha fomu za mgombea wake.
 
Alisema BLW limepokea fomu ya mgombea mmoja kutoka CCM, Zuberi Ali Maulid, ambaye amependekezwa na chama chake kuwania wadhifa huo.
 
Hamad alisema Baraza la Wawakilishi liliandikia Tume ya Uchaguzi Zanzibar (Zec) barua kuwa nafasi ya Spika ipo wazi na wao kuvitaarifu vyama vya siasa, lakini wameshindwa kujitokeza mpaka muda umemalizika wa kuchukua fomu na kurejesha.
 
Hata hivyo, alisema kuwa Tadea walichukua fomu ya kuwania wadhifa huo, lakini mpaka jana walishindwa kurejesha fomu ya mgombea wake, Rashid Mshenga.
 
Aidha, alisema kuwa Rais mpaka jana alikuwa bado hajasema lini atazindua Baraza la Wawakilishi baada ya kukamilika kwa uchaguzi mkuu wa marudio uliofanyika Machi 20, mwaka huu.
 
“Kazi kubwa kwa Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi baada ya kukutana, itakuwa kuchagua Spika, lakini Baraza halitakuwa na upinzani,” alisema Hamad.
 
Katika hatua nyingine, mgombea wa nafasi ya Spika kupitia CCM, Zuberi Ali Maulid, jana alirejesha fomu huku akitamba kuwa Baraza lake litakuwa na nguvu licha ya kukosekana kambi ya upinzani kwa mara ya kwanza tangu kuanzishwa mfumo wa vyama vingi nchini.
 
Waziri huyo wa zamani wa Miundombinu na Mawasiliano, anagombea wadhifa huo baada ya kumwagusha aliyekuwa Spika wa BLW, Pandu Ameir Kificho, katika uchaguzi wa chama kuwania wadhifa huo.
 
Zuberi alisema atakikisha anasimamia sheria na kanuni ili kuona chombo hicho kinatekeleza majukumu yake ya kuisimamia serikali na kuongeza uwajibikaji wake.
 
“Mambo yatakuwa mazuri bila ya kuwapo wapinzani, nitasimamia sheria na kanuni ili Baraza liisimamie serikali pamoja kero za wananchi kuona zinapatiwa majibu,” alisema Zuberi muda mfupi baada ya kurejesha fomu yake.
 
Wajumbe 72 wa Baraza la Wawakilishi wote kutoka CCM, leo wataanza kusajiliwa kabla ya Baraza kukutana huku wananchi wengi wakiwa na wasiwasi wa Baraza hilo kutokuwa na meno ya kuibana serikali kutokana na wajumbe wake kuwa wanatoka chama tawala cha CCM pekee.
 
Hali hiyo imetokana na CUF kususia uchaguzi mkuu wa marudio kwa madai uchaguzi wa awali wa Oktoba 25, mwaka jana ulikuwa huru na haki.
 
CHANZO: NIPASHE

Post a Comment

CodeNirvana
Newer Posts Older Posts
© Copyright NEWZ | Designed By AFROPIXELS MEDIA CO. LTD
Back To Top