Loading...

HIVI NDIVYO ALIVYOAPISHWA RAIS WA ZANZIBAR DR. SHEIN

Dk. Ali Mohamed Shein, Rais wa Awamu ya saba wa Zanzibar
DAKTARI Ali Mohammed Shein amekiomba radhi Chama cha Wananchi (CUF) kiaina wakati wa sherehe za kuapishwa kwake kuwa Rais wa Zanzibar leo kwenye Uwanja wa Aman Abeid Karume, Zanzibar, anaandika Happyness Lidwino.
Bila kutaja jina Dk. Shein amesema “uchaguzi umekwisha, tuache itikadi za vyama tushirikiane” kauli inayoilenga CUF kutokana na msimamo wake kwa kutoshirikiana na serikali yake.
CUF imetangaza kutoshiriki chochote katika serikali ya Dk. Shein baada ya Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC) kufuta matokeo halali ya Uchaguzi Mkuu uliofanyika tarehe 25 Machi mwaka jana.
Dk. Shein amesema, uchaguzi umeisha na kwamba, wananchi wanapaswa kuweka pembeni itikadi zao za vyama na kushirikiana naye katika kuiletea maendeleo Zanzibar.
Hata hivyo, Dk. Shein amewaeleza wananchi visiwani humo kwamba, hayupo tayari kuona amani ya visiwa hivyo inatoweka na kwamba atakayethubutu hatomvumilia.
“Lakini pia sitakubali na nitakuwa mkali kwa wale wote watakaokuwa kinyume na mimi watakaosababisha amani kutoweka sitawaacha, nitawashuhulikia,” amesema Dk. Shein.
Kwenye sherehe hizo Dk. Shein amesema kuwa, ushindi wake umekiongezea sifa chama chake na kwamba, atawatumikia wananchi wote bila upendeleo.
‘’Ushindi wetu umeongeza sifa kwa chama changu. Naahidi kuwatumikia wananchi wote pasipo upendeleo na kushirikiana na Serikali ya Tanzania Bara ili kudumisha amani na ushirikiano kama ilivyokuwa mwanzo,’’ amesema Dk. Shein.
Shein ameapishwa na Omar Othman Makungu, Jaji Mkuu wa Zanzibar akishuhudiwa na viongozi mbalimbali wa serikali na dini baada ya kutajwa kuchaguliwa kwa asilimia 91.
Baadhi ya viongozi wakuu waliohudhulia katika sherehe hizo ni pamoja na Rais John Magufuli; Samia Suluhu Hassan, Makamu wa Rais Tanzania; Kassim Majaliwa, Waziri Mkuu wa Tanzania na Abdurahman Kinana, Katika Mkuu wa CCM.
Mara baada ya kuapishwa Dk. Shein amewapongeza wagombea wenza walioshiriki katika mchakato wa uchaguzi kwa kuwa wavumilivu mwanzo mpaka mwisho.
Hadi alipokwenda kupiga kura Machi 20 mwaka huu, Dk. Shein alikuwa bado ni Rais wa Zanzibar na urais wake ulitenguliwa sekunde chache kabla ya Jecha Salim Jecha, Mwenyekiti wa ZEC kumtangaza kuwa rais mteule kwa awamu nyingine.

Post a Comment

CodeNirvana
Newer Posts Older Posts
© Copyright NEWZ | Designed By AFROPIXELS MEDIA CO. LTD
Back To Top