Loading...

Zanzibar ni kupe katika Muungano?

Dk. Ali Mohamed Shein, Rais wa Zanzibar
RAIS wa Jamhuri, Dk. John Pombe Magufuli, amefuta Sherehe za Maadhimisho ya Muungano. Ameagiza wananchi waadhimishe sherehe hizo wakiwa majumbani au katika shughuli zao binafsi,anaandika Saed Kubenea.
Sherehe za Muungano huadhimishwa tarehe 26 Aprili kila mwaka. Jamhuri ya Muungano inaundwa na nchi mbili – iliyokuwa Jamhuri ya Tanganyika na Jamhuri ya Watu wa Zanzibar.
Dk. Magufuli amesema kiasi cha Sh. 2 bilioni, zilizopangwa kutumika kugharimia vinywaji, vyakula, gwaride, halaiki na burudani, zitumike kwa upanuzi wa barabara jijini Mwanza.
Hii ni mara ya pili kwa rais kufuta sherehe za taifa tangu aapishwe kuwa rais.
Alianza kufuta sherehe za Uhuru wa Tanganyika. Hizi hufanyika tarehe 9 Desemba ya kila mwaka. Akatangaza siku hiyo itakuwa siku ya usafi ili kuondokana na alichoita, “ugonjwa wa kipindupindu unaoikabili nchi.”
Aliyekuwa Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue alisema, rais ameagiza wakuu wa mikoa na wilaya zote waandae vifaa vya usafi kwa ajili ya shughuli hiyo.
Ilielezwa kwamba bajeti iliyokuwa imeandaliwa kwa ajili ya sherehe hizo, itaelekezwa kwenye sekta nyingine yenye uhitaji.
Baadaye rais alitangaza kuwa fedha za sherehe za uhuru zimeelekezwa kwenye upanuzi wa barabara ya Bagamoyo. Tujadili:
Kwanza, hatua ya rais kufuta sherehe za Muungano au sherehe za uhuru, kwa kisingizio chochote kile haikubaliki. Hii ni kwa sababu, sherehe za uhuru katika taifa lolote lile siyo jambo dogo hata kidogo.
Taifa hili limekuwa huru kwa kuwa wazazi wetu, walikataa utumwa. Walitaka kuwa huru. Walikataa kutawaliwa na taifa lingine.
Waligoma kutawaliwa siyo kwa kuwa ni fedheha tu, bali ni sawa na kutuweka kwenye utumwa. Walikataa kuwa vijakazi wa kushangilia mabwana zao hata pale wanapofanya makosa.
Hii ni siku ambayo wimbo wa taifa huru la Tanganyika uliimbwa katika uwanja wa taifa. Machozi ya baba na mama zetu yalichuruzika kwa furaha isiyo kifani; huku wakimuaga aliyekuwa gavana, Sir Richard Gordon Turnbull na mume wa Malkia wa Uingereza, Prince Phillip.
Wote wawili walikuwapo uwanja wa taifa kushuhudia tukio hilo la kihistoria – uhuru wa Tanganyika.
Sherehe za uhuru siyo tu ishara ya kushusha bendera ya Uingereza na kupeperusha bendera ya Tanganyika; bali ni tendo la kuhitimisha juhudi za wapambanaji, wakiongozwa na Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, za kuleta utu wa Mwafrika; hivyo utu wa Mtanganyika.
Ni tendo la kujiondoa kwenye minyororo ya ukoloni – utumwa wa kisiasa na kiuchumi – na kuasisi fikra na matendo mapya ya kujiongoza na kujitawala bila shinikizo la watawala wengine kutoka nje ya nchi.
Wakati katika uwanja wa taifa, machozi ya wazazi wetu yakidondoka kwa furaha isiyomithilika, Luteni Alexander Nyirenda, ofisa wa jeshi mzalendo, alikuwa akisimika mwenge wa Uhuru na bendera ya Tanganyika huru, kwenye kilele cha Mlima Kilimanjaro.
Ndani ya uwanja wa taifa, baadhi ya maofisa wa jeshi la Uingereza walibadilishana bendera za majeshi – Tanganyika Rifles (TR) na King’s African Rifles (KAR).
Ijapokuwa tulipata uhuru bila kumwaga damu, lakini Mwalimu Nyerere na viongozi wenzake katika African National Union (TANU), walipata misukosuko.
Miaka miwili kabla ya uhuru, Mwalimu Nyerere alishitakiwa mahakamani kwa madai ya kuandika maneno ya kashfa kwenye gazeti (Crimanal libel), juu ya mzungu aliyekuwa mkuu wa wilaya. Alitetewa na mawakili kutoka Uingereza.
Historia ya aina hii, haiwezi kufutwa kwa visingizio vya kubana matumizi. Vinginevyo, kufuta sherehe hizi za kila kunalenga kudhalilisha kazi iliyofanywa na waliopigania uhuru huu.
Aidha, tunaitwa Watanzania, kwa sababu kuna Muungano kati ya Tanganyika na Zanzibar. Nje ya Muungano, kuna Watanganyika na Wanzanzibari.
Hivyo, kufuta sherehe za Muungano, ni kufuta historia ya taifa. Hata Ujerumani ambao walikuwa na uhasama mkubwa kati ya Mashariki na Magharibi, bado wanaendelea kusheherekea siku yao ya Muungano.
Pili, kuahirisha sherehe za Muungano kwa kisingizio cha kubana matumizi, kunaibua utamaduni mpya wa rais kujitwisha mamlaka ya Bunge.
Kwa mujibu wa sheria na Katiba ya Jamhuri ya Muungano, mwenye mamlaka ya kuhamisha fedha kutoka fungu moja kwenda jingine, ni Bunge. Siyo rais. Kama rais anataka kuhamisha fedha sharti alijulishe Bunge na lenyewe liridhie.
Rais anajua utaratibu wa kupitisha bajeti ya serikali bungeni. Kwamba Bunge hutenda kazi kwa niaba ya wananchi. Yeye mwenyewe alikuwa mbunge na waziri kwa miaka 15 akihudumu katika serikali ya Benjamin Mkapa na Jakaya Kikwete.
Anajua kuwa Bunge ndilo lenye kazi ya kukagua fedha ambazo zimetengwa kwa kila kasma ya serikali. Kupokonya mamlaka ya Bunge, ni kuvunja sheria, Katiba na kudhalilisha Mamlaka Kuu ambayo ni watu wa nchi hii.
Je, ikiwa fedha zinahamishwa kwa amri za rais, nani atazikagua? Yupi atakayewajibika ikiwa kutatokea ulaji?
Ikiwa fedha zinahamishwa kwa amri ya rais, nani atadhibiti watakaozitumia vibaya? Nani atamwajibisha rais kwa kuhamisha fedha huku na kupeleka kule?
Vilevile, kitendo cha rais wa upande mmoja wa Muungano, kuamuru fedha za sherehe za Muungano – jambo linalohusu nchi mbili ndani ya Jamhuri ya Muungano – zitumike upande mmoja (Tanganyika), ni kuifanya Zanzibar kuonekana siyo taifa huru ndani ya Muungano.
Fedha iliyotoka kwa ajili ya matumizi yanayohusu mataifa mawili yanayounda Muungano, inapoamuliwa kutumiwa na taifa moja; na bila taifa la pili kujulishwa au kupata sehemu ya fedha hizo, kunaweza kuingiza Muungano katika mgogoro.
Au ni kweli kuwa Zanzibar huwa haichangii lolote katika serikali ya Muungano? Kwamba fedha zimetoka Bara na baada ya sherehe kughairishwa zimebaki kwa waliotoa? Hili linasomekaje? Linasikikaje? Linaelewekaje?
Rais angeeleweka kama angesema, serikali haina fedha. Haina fedha za maandalizi ya sherehe na sherehe zenyewe. Siyo vibaya hata kidogo kwa serikali kusema ukweli, kama huo ni ukweli, kwamba haina fedha.
Kama serikali ingekuwa na fedha na kweli imetaka kuokoa fedha hizo kutumika kwa matumizi yasiyo ya lazima, mbona haikutangaza kupeleka fedha hizo kwa ajili ya wenye njaa – huko Bunda, mkoani Mara, ambako njaa imejenga maghorofa?
Mbona haitangazi kupeleka fedha hizo kwa waliopatwa na maafa; au wasio na mavazi ili wajisetiri.
Lakini kusema kwamba fedha za sherehe za Muungano zikatumike kujenga barabara ya Mwanza, wakati kazi ya kuhamisha fedha kutoka fungu moja kwenda jingine ni kazi ya Bunge, ni kujitafutia mgogoro na wananchi.

Post a Comment

CodeNirvana
Newer Posts Older Posts
© Copyright NEWZ | Designed By AFROPIXELS MEDIA CO. LTD
Back To Top